Tatizo Zito Sana: Usaliti (2)

Asili ya mwanadamu ni tofauti kabisa na kiini Changu, kwa sababu asili potovu ya mwanadamu hutoka kwa Shetani kabisa; asili ya mwanadamu imechakatwa na kupotoshwa na Shetani. Yaani, mwanadamu anaishi chini ya ushawishi wa uovu na ubaya wake. Mwanadamu hakui katika ulimwengu wa ukweli au mazingira matakatifu, sembuse mwanadamu kuishi katika nuru. Kwa hiyo, haiwezekani kwa mtu yeyote kuwa na ukweli ndani ya asili yake tangu wakati wa kuzaliwa, sembuse mtu kuweza kuzaliwa na kiini kinachomwogopa na kumtii Mungu. Badala yake, watu wana asili ambayo inampinga na kumwasi Mungu, na haipendi ukweli. Asili hii ndio tatizo Ninalotaka kujadili—usaliti. Usaliti ndio chanzo cha kila mtu kumpinga Mungu. Hili ni tatizo ambalo linapatikana ndani ya mwanadamu tu, na sio ndani Yangu. Wengine watauliza: Kwa kuwa watu wote wanaishi ulimwenguni jinsi tu Kristo aishivyo, mbona watu wote wana asili ambazo zinamsaliti Mungu, ilhali Kristo hana asili hiyo? Hili ni tatizo ambalo ni lazima mfafanuliwe kwa uwazi.

Msingi wa uwepo wa wanadamu ni kuzaliwa upya kwa nafsi tena na tena. Kwa maneno mengine, kila mtu hupata maisha ya kibinadamu katika mwili nafsi yake inapozaliwa upya. Baada ya mwili wa mtu kuzaliwa, maisha yake yanaendelea mpaka mwili utakapofikia ukomo wake, ambao ndio wakati wa mwisho, wakati nafsi inapoliacha ganda lake. Utaratibu huu hujirudia tena na tena, nafsi ya mtu inakuja na kuondoka mara kwa mara, na hivyo uwepo wa wanadamu unadumishwa. Maisha ya mwili pia ni maisha ya nafsi ya mwanadamu, na nafsi ya mwanadamu hukimu uwepo wa mwili wa mwanadamu. Hiyo ni kusema, maisha ya kila mtu hutoka kwenye nafsi yake, na maisha hayana asili katika mwili. Kwa hivyo, asili ya mwanadamu hutoka kwenye nafsi, si kutoka kwenye mwili. Ni nafsi ya kila mtu pekee ndiyo inayojua jinsi alivyopitia majaribu, mateso na upotovu wa Shetani. Mwili wa mwanadamu hauyajui mambo haya. Kwa hiyo, bila kujua, wanadamu wanakuwa waovu zaidi, wachafu zaidi, na wabaya zaidi, wakati umbali kati ya mwanadamu na Mimi unazidi kuwa mkubwa, na maisha yanakuwa yenye giza zaidi kwa wanadamu. Shetani anashikilia nafsi za wanadamu kwa nguvu, kwa hiyo, bila shaka, mwili wa mwanadamu pia umemilikiwa na Shetani. Mwili kama huo na wanadamu kama hao wangewezaje kutompinga Mungu? Je, wangewezaje kulingana na Yeye kiasili? Sababu iliyonifanya Nimtupe Shetani chini angani ni kwa sababu alinisaliti. Je, basi wanadamu wanawezaje kutohusishwa? Hii ndiyo sababu usaliti ni asili ya mwanadamu. Ninaamini kwamba mara tu mnapoelewa hoja hii, mnapaswa pia kuwa na imani katika kiini cha Kristo. Mwili uliovaliwa na Roho wa Mungu ni mwili wa Mungu mwenyewe. Roho wa Mungu ni mwenye mamlaka; Yeye ni mwenye uweza, mtakatifu, na mwenye haki. Vivyo hivyo, mwili Wake pia ni wenye mamlaka, wenye uweza, mtakatifu, na wenye haki. Mwili kama huo unaweza kufanya tu kile ambacho ni cha haki na chenye faida kwa wanadamu, kile ambacho ni kitakatifu, kitukufu na chenye nguvu; Yeye hawezi kutenda jambo lolote ambalo linakiuka ukweli, ambalo linakiuka maadili na haki, sembuse kufanya jambo lolote linaloweza kumsaliti Roho wa Mungu. Roho wa Mungu ni mtakatifu, na kwa hivyo mwili Wake hauwezi kupotoshwa na Shetani; mwili Wake ni wenye kiini tofauti na mwili wa mwanadamu. Kwa maana ni mwanadamu na si Mungu, ambaye anapotoshwa na Shetani; Shetani hawezi kamwe kuupotosha mwili wa Mungu. Kwa hiyo, licha ya ukweli kwamba mwanadamu na Kristo wanaishi katika sehemu sawa, ni mwanadamu tu ndiye anayemilikiwa, anayetumiwa, na anayenaswa na Shetani. Kinyume na hilo, Kristo hawezi kuathiriwa kabisa na upotovu wa Shetani, kwa sababu Shetani hatawahi kuweza kupanda hadi mahali pa juu zaidi, na hatawahi kuweza kumkaribia Mungu. Leo, nyote mnapaswa kuelewa kuwa ni wanadamu tu, waliopotoshwa na Shetani, ndio wanaonisaliti. Usaliti hautawahi kuwa suala linalomhusisha Kristo hata kidogo.

Nafsi zote zilizopotoshwa na Shetani zimeshikwa mateka katika miliki ya Shetani. Ni wale tu wanaomwamini Kristo ndio waliotengwa, waliookolewa kutoka katika kambi ya Shetani, na kuletwa ndani ya ufalme wa leo. Watu hawa hawaishi tena chini ya ushawishi wa Shetani. Hata hivyo, asili ya mwanadamu bado imekita mizizi katika mwili wa mwanadamu, yaani, ingawa nafsi zenu zimeokolewa, asili yenu bado ni sawa na ilivyokuwa hapo awali, na uwezekano kwamba mtanisaliti unabaki kuwa asilimia mia moja. Hii ndiyo sababu kazi Yangu inadumu kwa muda mrefu sana, kwa kuwa asili yenu haiwezi kudhibitiwa kwa urahisi. Sasa, ninyi nyote mnapitia magumu kadri ya uwezo wenu mnapotimiza wajibu wenu, ilhali kila mmoja wenu anaweza kunisaliti na kurudi katika miliki ya Shetani, kambini mwake, na kurudia maisha yenu ya zamani—huu ni ukweli usiopingika. Wakati huo, haitawezekana kwenu kudhihirisha chembe ya ubinadamu au mfano wa binadamu, kama mnavyofanya sasa. Katika hali mbaya zaidi, mtaangamizwa, na zaidi ya hayo, mtahukumiwa milele, mtaadhibiwa vikali, msizaliwe upya kamwe. Hili ndilo tatizo lililowekwa mbele yenu. Ninawakumbusha kwa njia hii, kwanza, ni ili kazi Yangu isiwe imekuwa ya bure, na pili, ni ili ninyi nyote muweze kuishi katika siku zenye nuru. Kwa kweli, kama kazi Yangu ni ya bure si tatizo kubwa sana. Jambo la muhimu sana ni kwamba mnaweza kuwa na maisha yenye furaha na mustakabali mzuri sana. Kazi Yangu ni kazi ya kuziokoa nafsi za watu. Nafsi yako ikianguka mikononi mwa Shetani, mwili wako hautaishi kwa amani. Ikiwa Ninaulinda mwili wako, hakika nafsi yako pia itakuwa chini ya uangalizi Wangu. Nikikuchukia sana, mwili na nafsi yako vitaanguka mikononi mwa Shetani mara moja. Je, unaweza kukisia hali yako kwa wakati huo? Ikiwa, siku moja mtayapuuza maneno Yangu, basi Nitawakabidhi nyote kwa Shetani, ambaye atawatesa sana hadi hasira Yangu itakapoisha kabisa, au Mimi binafsi Nitawaadhibu ninyi wanadamu msioweza kuokoleka, kwa kuwa mioyo yenu inayonisaliti haitakuwa imewahi kubadilika.

Nyote mnapaswa sasa kujichunguza haraka iwezekanavyo, ili muone ni kiasi gani cha usaliti wenu Kwangu umebaki ndani yenu. Ninangojea kwa shauku jibu lenu. Msiwe wazembe katika kushughulika na Mimi. Kamwe Mimi huwa sichezi michezo na watu. Nikisema Nitafanya jambo basi kwa hakika Nitalifanya. Natumai kila mmoja wenu ataweza kuwa mtu ambaye anayachukulia maneno Yangu kwa uzito, na asifikirie ni kana kwamba maneno hayo ni ubunifu wa kisayansi. Kile Ninachotaka ni matendo ya wazi kutoka kwenu, siyo mawazo yenu. Kisha, ni lazima myajibu maswali Yangu, ambayo ni kama yafuatavyo:

1. Ikiwa kwa kweli wewe ni mtendaji huduma, je, unaweza kutoa huduma Kwangu kwa uaminifu, bila dalili yoyote ya uzembe au mtazamo hasi?

2. Je, ukigundua kuwa Sijawahi kukuthamini, bado utaweza kusalia na kunitolea huduma kwa maisha yako?

3. Ikiwa bado Sifanyi chochote kwako licha ya wewe kutumia bidii nyingi, je, utaweza kuendelea kunifanyia kazi katika hali ya mashaka?

4. Ikiwa, baada ya wewe kujitumia kwa ajili Yangu, Siyaridhishi mahitaji yako madogo, je, utavunjika moyo na kusikitishwa na Mimi, au hata ukasirike na kunitukana kwa sauti kubwa?

5. Ikiwa daima umekuwa mwaminifu sana, ukinipenda sana, lakini bado unateseka na ugonjwa, umaskini, na kutengwa na marafiki na jamaa zako, au ikiwa unavumilia taabu nyingine zozote maishani, je, bado uaminifu na upendo wako Kwangu utaendelea?

6. Ikiwa hakuna lolote kati ya yale ambayo umefikiria moyoni mwako linalingana na kile ambacho Nimefanya, je, utaitembea vipinjia yako ya baadaye?

7. Ikiwa hupokei chochote kati ya mambo ambayo ulitarajia kupokea, je, unaweza kuendelea kuwa mfuasi Wangu?

8. Ikiwa hujawahi kuelewa dhumuni na umuhimu wa kazi Yangu, je, unaweza kuwa mtu mtiifu ambaye hatoi hukumu kiholela na kufanya maamuzi?

9. Je, unaweza kuthamini maneno yote ambayo Nimeyanena na kazi yote ambayo Nimeifanya wakati Nimekuwa pamoja na wanadamu?

10. Je, unaweza kuwa mfuasi Wangu mwaminifu, aliye tayari kuvumilia mateso ya maisha kwa ajili Yangu, ingawa hupokei chochote?

11. Kwa ajili Yangu, je, unaweza kuacha kufikiria, kupanga, au kutayarisha njia yako ya baadaye ya kuishi?

Maswali haya yanawakilisha mahitaji Yangu ya mwisho Ninayotaka kutoka kwenu, nami Natumai kuwa ninyi nyote mnaweza kunipa majibu. Ikiwa umetimiza jambo moja au mawili ambayo maswali haya yanataka ufanye, basi lazima uendelee kujitahidi. Ikiwa huwezi kutimiza hata moja kati ya mahitaji haya, hakika wewe ni aina ya mtu ambaye atatupwa kuzimu. Sihitaji kusema chochote zaidi kwa watu kama hawa, kwani kwa hakika wao sio watu ambao wanaweza kupatana na Mimi. Je, Ninawezaje kumweka nyumbani Kwangu mtu ambaye anaweza kunisaliti katika hali yoyote ile? Kwa wale ambao bado wanaweza kunisaliti katika hali nyingi, Nitazingatia utendaji wao kabla ya kufanya mipango mingine. Hata hivyo, wote wanaoweza kunisaliti, bila kujali ni chini ya hali gani, Sitasahau kamwe; Nitawakumbuka moyoni Mwangu, na kungojea fursa ya kuwalipa matendo yao maovu. Mahitaji yote ambayo Nimeibua ni shida ambazo lazima nyote mzichunguze ndani yenu wenyewe. Natumai kuwa ninyi nyote mtaweza kuyazingatia kwa makini na msishughulike na Mimi kwa uzembe. Hivi karibuni, Nitaangalia majibu ambayo mmenipa dhidi ya mahitaji Yangu. Kufikia wakati huo, Sitahitaji chochote zaidi kutoka kwenu na Sitawapa onyo la dhati zaidi. Badala yake, Nitatumia mamlaka Yangu. Wale wanaopaswa kuhifadhiwa watahifadhiwa, wale wanaopaswa kupewa thawabu watapewa thawabu, wale wanaopaswa kukabidhiwa kwa Shetani watakabidhiwa kwa Shetani, wale wanaopaswa kuadhibiwa vikali wataadhibiwa vikali, na wale wanaopaswa kuangamia wataangamizwa. Kwa hivyo, hakutakuwa tena na mtu wa kunisumbua katika siku Zangu. Je, unayaamini maneno Yangu? Je, unaamini kulipiza kisasi? Je, unaamini kuwa Nitawaadhibu wale waovu wote wanaonidanganya na kunisaliti? Je, unatarajia siku hiyo ije kwa haraka au ije baadaye? Je, wewe ni mtu ambaye anaogopa adhabu, ama ni mtu ambaye angenipinga ingawa lazima avumilie adhabu? Siku hiyo itakapowadia, je, unaweza kukisia ikiwa utaishi katikati ya shangwe na kicheko, au ikiwa utalia na kusaga meno yako? Je, unatarajia kukumbana na mwisho wa aina gani? Je, umewahi kufikiria kwa uzito ikiwa unaniamini Mimi kwa asilimia mia moja au una mashaka Nami kwa asilimia mia moja? Je, umewahi kufikiria kwa makini ni athari na matokeo ya aina gani ambayo matendo na tabia yako itakuletea? Je, unatumaini kwa kweli kuwa maneno Yangu yote yatatimizwa moja baada ya jingine, ama unaogopa kuwa maneno Yangu yatatimizwa moja baada ya jingine? Ikiwa unatumaini kuwa Nitaondoka hivi karibuni ili Niyatimize maneno Yangu, je, unapaswa kuyachukuliaje maneno na matendo yako mwenyewe? Ikiwa hautumaini kuondoka Kwangu na hautumaini maneno Yangu yote yatimizwe mara moja, kwa nini uniamini Mimi hata kidogo? Je, unajua kweli ni kwa nini unanifuata Mimi? Ikiwa sababu yako ni kupanua upeo wako tu, hakuna haja ya kujisumbua kufanya hivyo. Ikiwa ni ili ubarikiwe na kuepukana na msiba unaokuja, mbona hujali kuhusu tabia yako mwenyewe? Mbona hujiulizi ikiwa unaweza kuyakidhi mahitaji Yangu? Mbona pia hujiulizi ikiwa unastahili kupokea baraka zitakazokuja?

Iliyotangulia:  Tatizo Zito Sana: Usaliti (1)

Inayofuata:  Mnapaswa Kuzingatia Matendo Yenu

Mipangilio

  • Matini
  • Mada

Rangi imara

Mada

Fonti

Ukubwa wa Fonti

Nafasi ya Mstari

Nafasi ya Mstari

Upana wa ukurasa

Yaliyomo

Tafuta

  • Tafuta Katika Maneno Haya
  • Tafuta Katika Kitabu Hiki

Connect with us on Messenger