Ni Wale tu Wanaomjua Mungu na Kazi Yake Ndio Wanaoweza Kumridhisha Mungu

Kazi ya Mungu mwenye mwili inajumuisha sehemu mbili. Mara ya kwanza Alipofanyika mwili, watu hawakumwamini au kumfahamu na wakamsulubisha Yesu msalabani. Mara ya pili, pia, watu hawakumwamini, sembuse kumfahamu, na kwa mara nyingine tena wakamsulubisha Kristo msalabani. Je, mwanadamu si adui wa Mungu? Kama mwanadamu hamjui Yeye, mwanadamu anawezaje kuwa mwandani wa Mungu? Na anawezaje kuwa na sifa za kumshuhudia Mungu? Je, si madai ya kumpenda Mungu, kumtumikia Mungu, kumtukuza Mungu yote ni udanganyifu? Kama unayatoa maisha yako kwa haya mambo yasiyokuwa na uhalisi, yasiyoweza kutekelezeka, huoni kama unafanya kazi bure? Unawezaje kuwa mwandani wa Mungu wakati hujui Mungu ni nani? Kufuatilia kama huko si kusio dhahiri na kwa dhahania? Je, sio kwa udanganyifu? Mtu anawezaje kuwa mwandani wa Mungu? Kuna maana gani kivitendo kuwa mwandani wa Mungu? Je, unaweza kuwa mwandani wa Roho wa Mungu? Je, unaweza kuona jinsi Roho alivyo mkubwa na alivyoinuliwa? Kuwa mwandani wa Mungu asiyeonekana, asiyeshikika—hili si jambo lisilo dhahiri na la dhahania? Maana ya utendaji ya kufuatilia huku ni gani? Je, sio udanganyifu mtupu tu? Kile unachokifuatilia ni kuwa mwandani wa Mungu, lakini bado ni mtumwa wa Shetani, maana humfahamu Mungu, na kumfuatilia “Mungu wa vitu vyote,” asiyekuwepo ambaye haonekani, hashikiki, na ni wa dhana zako mwenyewe. Kwa maana isiyo dhahiri, huyo “Mungu” ni Shetani, na kwa uhalisi, ni wewe mwenyewe. Unatafuta kuwa mwandani wako mwenyewe halafu bado unasema unatafuta kuwa mwandani wa Mungu—huko si ni kukufuru? Thamani ya ufutiliaji wa aina hii ni nini? Kama Roho wa Mungu hawezi kuwa mwili, basi kiini cha Mungu ni kitu kisichoonekana, Roho wa uzima asiyeshikika, asiyekuwa na umbo, hana vitu vya kushikika, hafikiki na mwanadamu hawezi kumtambua. Mwanadamu anawezaje kuwa mwandani wa Roho asiyekuwa na mwili, wa ajabu na asiyeweza kueleweka kama huyu? Huu sio utani? Fikira ya kipuuzi kama hiyo ni batili na haitekelezeki. Mwanadamu aliyeumbwa kwa asili yuko tofauti na Roho wa Mungu, sasa inawezekanaje wawili hawa kuwa wandani? Ikiwa Roho wa Mungu hakutambuliwa katika mwili, ikiwa Mungu hakuwa mwili na kujishusha Mwenyewe kwa kufanyika kiumbe, basi mwanadamu aliyeumbwa asingekuwa na sifa na kuwa na uwezo wa kuwa mwandani Wake, na licha ya wachamungu ambao wanaweza kuwa na nafasi ya kuwa wandani wa Mungu baada ya Roho zao kuingia mbinguni, watu wengi wasingeweza kuwa wandani wa Roho wa Mungu. Na ikiwa mwanadamu anataka kuwa mwandani wa Mungu mbinguni chini ya uongozi wa Mungu mwenye mwili, je, yeye si mwanadamu mpumbavu kupindukia? Mwanadamu anakuwa tu “mwaminifu” kwa Mungu asiyeonekana, na wala hamzingatii Mungu ambaye anaweza kuonekana, kwa maana ni rahisi sana kumfuata Mungu asiyeonekana—mwanadamu anaweza kufanya hivyo kwa vyovyote apendavyo. Lakini njia ya Mungu anayeonekana si rahisi. Mwanadamu ambaye anamtafuta Mungu asiye dhahiri hakika hawezi kumpata Mungu, maana vitu ambavyo si dhahiri na ni vya dhahania vyote vinafikiriwa na mwanadamu, na ambavyo mwanadamu hawezi kuvipata. Ikiwa Mungu ambaye alikuja kwenu angekuwa Mungu wa kifahari na aliyeinuliwa ambaye angekuwa hafikiki kwenu, sasa mngewezaje kutafuta mapenzi Yake? Na mngewezaje kumfahamu na kumwelewa? Ikiwa angefanya kazi Yake tu, na wala hakuwa na uhusiano na mwanadamu, au hakuwa na ubinadamu wa kawaida na hakuweza kufikiwa na mwanadamu mwenye mwili wa kufa, basi, hata kama Alifanya kazi kubwa kwa ajili yako, lakini hukuweza kuhusiana naye, na hukuweza kumwona, utawezaje kumfahamu? Kama isingekuwa kwa kuchukua mwili wa ubinadamu, mwanadamu asingeweza kumjua Mungu; ni kwa sababu tu ya Mungu mwenye mwili ndiyo mwanadamu amestahili kuwa mwandani wa Mungu mwenye mwili. Mwanadamu huwa mwandani wa Mungu kwa sababu mwanadamu huhusiana naye, kwa sababu mwanadamu huishi naye na kuambatana naye, na kwa hivyo huja kumjua. Isingekuwa hivyo mwanadamu kumtafuta Mungu si kungekuwa ni bure? Hiyo ni kusema, si kwa sababu ya kazi ya Mungu ndiyo mwanadamu anaweza kuwa mwandani wa Mungu, bali ni kwa sababu ya uhalisi na ukawaida wa Mungu mwenye mwili. Ni kwa sababu tu Mungu huwa mwili ndiyo mwanadamu huwa na nafasi ya kufanya wajibu wake, na nafasi ya kumwabudu Mungu wa kweli. Je, si huu ni ukweli halisi na unaoweza kutekelezeka? Sasa, bado unatamani kuwa mwandani wa Mungu mbinguni? Ni pale tu ambapo Mungu anajinyenyekeza kwa kiwango fulani, ambayo ni kusema, ni wakati tu ambapo Mungu anafanyika mwili, ndipo mwanadamu anaweza kuwa mwandani na msiri Wake. Mungu ni wa Roho: Mwanadamu anawezaje kuwa na sifa ya kuwa mwandani wa Roho huyu, ambaye ameinuliwa sana na asiyeweza kueleweka? Ni pale tu ambapo Roho wa Mungu anaposhuka na kuwa mwili, anakuwa kiumbe anayefanana na mwanadamu, ndipo mwanadamu huweza kuelewa mapenzi Yake na kimsingi kumilikiwa naye. Anazungumza na kufanya kazi katika mwili, kushiriki katika furaha, huzuni, na taabu za mwanadamu, Anaishi katika ulimwengu sawa na mwanadamu, Anamlinda mwanadamu, na kumwongoza, na kupitia hili Anamtakasa mwanadamu, na kumruhusu mwanadamu kupata wokovu Wake na baraka Zake. Baada ya kuvipata vitu hivi, mwanadamu hupata kuyaelewa mapenzi ya Mungu kwa kweli, na ni hapo tu ndipo anaweza kuwa mwandani wa Mungu. Hii ndiyo inaweza kutekelezeka. Ikiwa Mungu angekuwa asiyeonekana na asiyeshikika kwa mwanadamu, mwanadamu angewezaje kuwa mwandani Wake? Je, hili si fundisho tupu?

Wakiwa wamemwamini Mungu hadi sasa, watu wengi bado wanafuata yale yasiyoeleweka na ya kidhahania. Hawana uelewa wa uhalisi wa kazi ya Mungu leo, na bado wanaishi miongoni mwa nyaraka na mafundisho. Aidha, wengi bado hawajaingia katika uhalisi wa mafungu mapya ya maneno kama vile “kizazi kipya cha wale wanaompenda Mungu,” “mwandani wa Mungu,” “kielelezo na mfano wa kuigwa katika upendo wa Mungu,” “mtindo wa Petro”; badala yake yale wanayoyatafuta bado ni yasiyoeleweka na ya kidhahania, bado wanazunguka katika mafundisho, na hawana ufahamu wa uhalisi wa maneno haya. Roho wa Mungu anapokuwa mwili, unaweza kuona na kuigusa kazi Yake katika mwili. Lakini ikiwa bado huwezi kuwa mwandani Wake, kama bado huwezi kuwa msiri Wake, sasa basi utawezaje kuwa msiri wa Roho wa Mungu? Kama humfahamu Mungu wa leo, unawezaje kuwa mmoja wa kizazi kipya kinachompenda Mungu? Je, hizi si barua na mafundisho tupu? Je, unaweza kumwona Roho na kuhisi mapenzi Yake? Si haya ni maneno matupu? Haitoshi wewe kusema tu mafungu ya maneno na maneno haya, wala huwezi kupata kibali cha Mungu kupitia azimio pekee. Unatosheka na kusema maneno haya pekee, na unafanya hivyo ili kukidhi matamanio yako mwenyewe, kukidhi mitazamo yako isiyokuwa na uhalisi, na kutosheleza dhana na mawazo yako mwenyewe. Kama humfahamu Mungu wa leo, basi, bila kujali kile unachofanya, hutaweza kuuridhisha moyo wa Mungu. Kuwa msiri wa Mungu kuna maana gani? Bado huelewi hili? Kwa kuwa mwandani wa Mungu ni mwanadamu, hivyo Mungu pia ni mwanadamu, yaani, Mungu amekuwa mwili, amekuwa mwanadamu. Ni wale tu walio wa aina moja ndio wanaoweza kuitana wasiri, baada ya hapo ndipo tu ndio wanaweza kuchukuliwa kuwa ni wandani. Kama Mungu angekuwa wa Roho, mwanadamu aliyeumbwa angewezaje kuwa mwandani Wake?

Imani yako kwa Mungu, ufuatiliaji wako wa ukweli, na hata jinsi unavyojiendesha vyote vinapaswa kutegemea uhalisi: Kila kitu unachofanya kinapaswa kuwa cha vitendo, na hupaswi kufuata mambo hayo ya uwongo, ya kidhahania tu. Hakuna maana yoyote katika kufanya vitu namna hii, na, aidha, maisha kama hayo hayana maana. Kwa sababu njia yako na maisha havijengwi katika kitu chochote kile isipokuwa uongo na ulaghai, na hufuati vitu ambavyo vina thamani na maana, kitu pekee unachopata ni fikira za kipuuzi tu na mafundisho ambayo hayana ukweli. Vitu kama hivyo havina uhusiano na maana na thamani ya uwepo wako, na vinaweza tu kukuleta katika ulimwengu ulio tupu. Kwa namna hii, maisha yako yote yatakuwa hayana maana au thamani—na kama hufuatilii maisha yenye maana, basi unaweza kuishi mamia ya miaka na yote hiyo inaweza kuwa haina maana yoyote. Hayo yanawezaje kuitwa maisha ya mwanadamu? Haya hakika si ni maisha ya mnyama? Kwa namna hiyo hiyo, kama mtajaribu kufuata njia ya imani katika Mungu, na wala msijaribu kumfuata Mungu anayeweza kuonekana, na badala yake mumwabudu Mungu asiyeonekana na asiyeshikika, basi si kufuatilia kama huko ni bure? Mwisho wake, ufuatiliaji wako kutakuwa ni anguko kubwa. Kufuatilia kwa aina hiyo kuna manufaa gani kwako? Tatizo kubwa zaidi la mwanadamu ni kwamba anaweza kupenda tu vitu ambavyo hawezi kuviona au kuvigusa, vitu ambavyo ni vya siri kubwa na vya kushangaza, na kwamba haviwezi kufikiriwa na mwanadamu na haviwezi kufikiwa na mwanadamu. Kadiri vitu hivi vinavyokuwa si halisi, kadiri vinavyochambuliwa na mwanadamu, ambaye anavifuata bila kujali kitu chochote, na hujaribu kuvipata. Kadiri vinavyokuwa si halisi, ndivyo mwanadamu anavyozidi kuvichunguza na kuvichambua zaidi, hata kwenda kwa kiwango cha kufanya mawazo yake ya kina kuyahusu. Kinyume chake, jinsi vitu vinavyokuwa halisi zaidi, ndivyo mwanadamu anavyozidi kuvipuuza; huviangalia kwa dharau, na hata huvitweza. Huu hasa si mtazamo wenu juu ya kazi halisi Ninayoifanya leo? Kadiri mambo hayo yanavyokuwa halisi, ndivyo unavyozidi kuyadharau. Wala hutengi muda kwa ajili ya kuyachunguza, bali unayapuuza; unayadharau mambo haya halisi yenye kiwango cha chini, yenye matakwa ya moja kwa moja, na hata unakuwa na fikira nyingi kuhusu Mungu huyu ambaye ni halisi sana, na huwezi kuukubali kiurahisi uhalisi na ukawaida Wake. Kwa njia hii, huamini katika hali isiyo dhahiri? Una imani thabiti katika Mungu asiye dhahiri wa wakati uliopita, na wala hupendi kumjua Mungu wa kweli wa leo. Je, hii si kwa sababu Mungu wa jana na Mungu wa leo wanatoka enzi mbili tofauti? Je! si pia kwa sababu Mungu wa jana ndiye Mungu aliyeinuliwa wa mbinguni, ilhali Mungu wa leo ni mwanadamu mdogo duniani? Aidha, si pia kwa sababu Mungu anayeabudiwa na mwanadamu ni yule aliyetokana na dhana zake, wakati Mungu wa leo ni mwili halisi uliotengenezwa duniani? Hata hivyo, si kwa sababu Mungu wa leo ni halisi sana kiasi kwamba mwanadamu hamfuatilii? Maana kile ambacho Mungu wa leo anamtaka mwanadamu afanye ni kile ambacho mwanadamu hayupo radhi kabisa kukifanya, na ambacho kinamfanya ahisi aibu. Huku sio kufanya mambo yawe magumu kwa mwanadamu? Je, hili halionyeshi makovu yake hapa? Kwa namna hii, watu wengi hawamfuatilii Mungu wa kweli, Mungu wa vitendo, na kwa hivyo wanakuwa maadui wa Mungu mwenye mwili, yaani, wapinga Kristo. Huu si ukweli dhahiri? Hapo awali, wakati Mungu alikuwa bado hajafanyika mwili, unaweza kuwa ulikuwa mtu wa kidini, au mwamini mcha Mungu. Baada ya Mungu kuwa mwili, wacha Mungu wengi kama hao waligeuka bila kujua na kuwa wapinga Kristo. Unajua ni nini kinachoendelea hapa? Katika imani yako kwa Mungu, huzingatii uhalisi au kuufuatilia ukweli, lakini badala yake huzingatia uwongo—je, hiki si chanzo cha wazi zaidi cha uadui wako kwa Mungu mwenye mwili? Mungu mwenye mwili anaitwa Kristo, kwa hivyo wale wote wasiomwamini Mungu mwenye mwili si wapinga Kristo? Je, yule unayemwamini na kumpenda ni huyu Mungu mwenye mwili kweli? Je, kweli ni huyu Mungu aliye hai ambaye ni wa halisi zaidi na ambaye ni wa kawaida kabisa? Malengo ya ufuatiliaji wako, yako wapi hasa? Yako mbinguni au duniani? Je, ni dhana au ni ukweli? Je, ni Mungu au ni kiumbe fulani asiyekuwa wa kawaida? Kwa kweli, ukweli ndio halisi zaidi katika methali zote za maisha, na ni mkuu kabisa kuliko methali hizo miongoni mwa wanadamu wote. Kwa sababu ni matakwa ambayo Mungu anayataka kwa mwanadamu, na ni kazi ambayo inafanywa na Mungu mwenyewe, hivyo inaitwa methali ya maisha. Sio methali iliyoundwa kutoka katika kitu fulani, wala si nukuu maarufu kutoka kwa mtu maarufu; badala yake, ni matamshi kwa mwanadamu kutoka kwa Bwana wa mbingu na nchi na vitu vyote, na sio maneno fulani yaliyotolewa na mwanadamu, bali ni maisha asili ya Mungu. Na hivyo unaitwa ni methali ya juu kabisa kupita methali zote za maisha. Ufuatiliaji wa mwanadamu wa kuweka ukweli katika matendo ni kufanya wajibu wake, yaani, ufuatiliaji wa kukidhi matakwa ya Mungu. Asili ya matakwa haya ni ukweli halisi, badala ya mafundisho yasiyokuwa na maana ambayo hayafikiwi na mwanadamu yeyote. Kama kufuatilia kwako ni mafundisho tu na bila uhalisi wowote, huoni unaasi dhidi ya ukweli? Wewe si mtu anayeushambulia ukweli? Mtu wa namna hiyo anawezaje kufuatilia kumpenda Mungu? Watu ambao hawana uhalisi ni wale ambao wanausaliti ukweli, na wote kwa asili ni waasi!

Bila kujali jinsi unavyofuatilia, lazima, zaidi ya yote, uelewe kazi ambayo Mungu hufanya leo, na lazima ujue umuhimu wa kazi hii. Ni lazima uelewe na kujua ni kazi gani ambayo Mungu huleta Anapokuja katika siku za mwisho, ni tabia gani Anayoleta, na ni nini kitakachofanywa kikamilifu ndani ya mwanadamu. Ikiwa hujui au huelewi kazi ambayo Amekuja kufanya katika mwili, basi unawezaje kufahamu mapenzi Yake, na unawezaje kuwa mwandani Wake? Kwa kweli, kuwa mwandani wa Mungu si vigumu, lakini pia si rahisi. Iwapo watu wanaweza kulielewa kikamilifu na kuliweka katika vitendo, basi linakuwa si gumu; ikiwa watu hawawezi kuielewa vilivyo, basi inakuja kuwa ngumu zaidi, na, zaidi, wanakuwa rahisi kuwa na ufuatiliaji wao unawafanya wawe wasio yakini. Ikiwa, katika kumfuatilia Mungu, mwanadamu hana msimamo wake wa kusimamia, na hajui ni ukweli gani anapaswa kuufuata, basi ina maana kwamba hana msingi, na hivyo si rahisi kwake kusimama imara. Leo, kuna wengi ambao hawauelewi ukweli, ambao hawawezi kutofautisha kati ya wema na uovu au kipi cha kupenda na kipi cha kuchukia. Watu kama hawa ni vigumu kusimama imara. Ufunguo wa imani katika Mungu ni kuweza kuweka ukweli katika vitendo, kujali mapenzi ya Mungu, kujua kazi ya Mungu kwa mwanadamu Anapokuja katika mwili na kanuni ambazo kwazo Anazungumza; usifuate umati, na lazima uwe na kanuni katika kile unachopaswa kukiingia, na lazima uzishike. Kuyashikilia imara mambo ambayo yameangaziwa na Mungu kwako ni msaada kwako. Usipofanya hivyo, leo utakwenda njia moja, kesho utakwenda njia nyingine, na hutapata kitu chochote halisi. Kuwa hivi hakuna manufaa yoyote katika maisha yako. Wale ambao hawauelewi ukweli siku zote wanawafuata wengine. Ikiwa watu wanasema kwamba hii ni kazi ya Roho Mtakatifu, basi, wewe pia utasema ni kazi ya Roho Mtakatifu; ikiwa watu watasema ni kazi ya roho mchafu, basi wewe pia utatilia mashaka, au utasema ni kazi ya roho mchafu. Siku zote unakuwa kama kasuku kwa maneno ya wengine, na huwezi kutofautisha kitu chochote wewe mwenyewe, wala huwezi kufikiria mwenyewe. Huyu ni mtu ambaye hana msimamo, ambaye hana uwezo wa kutofautisha—mtu wa aina hiyo ni masikini asiye na thamani. Wewe siku zote hurudia maneno ya wengine: Leo inasemwa kuwa hii ni kazi ya Roho Mtakatifu, lakini kuna uwezekano siku moja mtu atasema si kazi ya Roho Mtakatifu, na si chochote bali matendo ya mwanadamu—na bado huwezi kuelewa, na utakaposhuhudia watu wengine wanasema hivyo, nawe pia unasema kitu kile kile. Kwa kweli ni kazi ya Roho Mtakatifu, lakini unasema ni kazi ya mwanadamu; hujawa mmoja wa wale wanaoikufuru kazi ya Roho Mtakatifu? Katika hili, hujampinga Mungu kwa sababu huwezi kutofautisha? Nani ajuaye, labda siku moja mtu atatokea na kusema “hii ni kazi ya roho mchafu,” na utakaposikia maneno haya utapotea, na kwa mara nyingine tena unafungwa na maneno ya wengine. Kila wakati mtu anapochochea usumbufu huwezi kusimama katika msimamo wako, na hii ni kwa sababu huna ukweli ndani yako. Kuamini katika Mungu na kutafuta maarifa ya Mungu si jambo rahisi. Hayawezi kupatikana kwa kukusanyika pamoja na kusikiliza mahubiri, na huwezi kukamilishwa na shauku pekee. Lazima upitie uzoefu, na ujue, na kuongozwa na kanuni katika matendo yako, na kupata kazi za Roho Mtakatifu. Utakapopitia katika uzoefu, utakuwa na uwezo wa kutofautisha mambo mengi—utakuwa na uwezo wa kutofautisha kati ya mema na mabaya, kati ya haki na uovu, kati ya kile ambacho ni cha mwili na damu na kile ambacho ni cha kweli. Unapaswa kuwa na uwezo wa kutofautisha kati ya mambo haya yote, na kwa kufanya hivyo, haijalishi ni mazingira gani, hutapotea kamwe. Hiki tu ndicho kimo chako halisi.

Kuijua kazi ya Mungu si jambo rahisi. Unapaswa kuwa na viwango na malengo katika utafutaji wako, unapaswa kujua jinsi ya kutafuta njia ya kweli, na jinsi ya kupima kujua kama ni njia ya kweli au si ya kweli, na kama ni kazi ya Mungu au kinyume chake. Kanuni ya msingi kabisa katika kuutafuta ukweli ni nini? Unapaswa kuangalia kama kuna kazi ya Roho Mtakatifu au la kwa njia hii, iwapo maneno haya ni maonyesho ya ukweli, yanamshuhudia nani, na ni kitu gani yanaweza kukupatia. Kutofautisha kati ya njia ya kweli na hizi njia za uongo kunahitaji njia kadhaa za maarifa ya msingi, ya msingi kabisa kati ya zote ni kusema iwapo kuna Kazi ya Roho Mtakatifu au la. Maana kiini cha imani ya mwanadamu katika Mungu ni imani katika Roho Mtakatifu. Hata imani yake katika Mungu mwenye mwili ni kwa sababu mwili huu ni mfano halisi wa Roho wa Mungu, ikiwa na maana kwamba imani hiyo bado ni imani katika Roho. Kuna tofauti kati ya Roho na mwili, lakini kwa kuwa mwili unatokana na Roho, na ndio Neno linakuwa mwili, hivyo kile ambacho mwanadamu anaamini katika ni uungu halisi wa Mungu. Hivyo, katika kutofautisha kama ni njia sahihi au la, zaidi ya yote ni sharti uangalie iwapo ina kazi ya Roho Mtakatifu au la, na baada ya hapo ni sharti uangalie kama kuna ukweli katika njia hii. Ukweli, kama unavyoitwa, ni tabia ya maisha ya ubinadamu wa kawaida. Kwa maneno mengine, ndicho kile ambacho kilihitajika kwa mwanadamu Mungu alipomuumba hapo mwanzo, yaani, ubinadamu a kawaida kwa ukamilifu (ikiwa ni pamoja na mantiki, umaizi, hekima, na maarifa ya msingi ya ya kibinadamu ya jinsi ya kutenda). Yaani, unapaswa kuangalia iwapo njia hii inaweza kuwaelekeza watu kuingia katika maisha ya kawaida ya binadamu, iwapo ukweli unaozungumziwa unafanya matakwa kulingana na uhalisi wa ubinadamu wa kawaida au la, iwapo ukweli huu ni halisi na wa kiutendaji au lai, na iwapo ni wa wakati muafaka au la. Ikiwa kuna ukweli, basi unaweza kuwaongoza watu kuingia katika upitiaji wa utendaji; zaidi ya hayo, watu wanakuwa wa kawaida zaidi, hisia zao kawaida za kibinadamu zinakuwa kamili zaidi, maisha yao katika mwili na maisha ya kiroho yanakuwa yampangilio zaidi, na mihemko yao inakuwa ya kawaida kabisa. Hii ni kanuni ya pili. Kuna kanuni nyingine moja zaidi, ambayo ni iwapo watu wana maarifa yanayoongezeka ya Mungu au la, na kama kupitia au kutopitia kazi kama hiyo na ukweli kunaweza kuhamasisha upendo wa Mungu ndani yao na kuwaleta karibu zaidi na Mungu. Katika hili, inaweza kupimwa iwapo ni njia sahihi au la. Kanuni ya msingi ni iwapo njia hii ni ya uhalisi badala ya kuwa ya kimiujiza, na iwapo inaweza kutoa maisha ya mwanadamu. Kama inakubaliana na kanuni hizi, hitimisho linaweza kuwekwa kwamba njia hii ni njia ya kweli. Ninasema maneno haya si kuwafanya mkubali njia nyingine katika uzoefu mtakaoupitia baadaye, wala si utabiri kwamba kutakuwa na kazi ya enzi nyingine mpya hapo baadaye. Ninayasema ili mweze kuwa na uhakika kwamba kazi ya leo ni kazi ya kweli, ili kwamba msiwe na uhakika nusu katika imani yenu katika kazi ya leo na kushindwa kuielewa kwa ndani. Kuna hata watu wengi ambao, licha ya kuwa na uhakika, bado wanafuata kwa mkanganyiko; uhakika kama huo hauna kanuni, na wanapaswa kuondolewa siku moja. Hata wale ambao wapo motomoto katika imani yao wanakuwa na uhakika katika mambo matatu na mambo matano wanakuwa hawana uhakika, kitu kinachoonyesha kuwa hawana msingi. Kwa sababu tabia yenu ni dhaifu sana na msingi wenu hauna kina, hivyo hamna uelewa wa kutofautisha. Mungu harudii kazi Yake, Hafanyi kazi ambayo si halisi, Hamtaki mwanadamu afanye mambo zaidi ya uwezo wake, na Hafanyi kazi ambayo inazidi akili ya mwanadamu. Kazi yote Anayofanya ipo ndani ya mawanda ya akili ya kawaida ya mwanadamu, na haizidi ufahamu wa ubinadamu wa kawaida, na kazi Yake ni kulingana na mahitaji ya kawaida ya mwanadamu. Ikiwa ni kazi ya Roho Mtakatifu, mwanadamu anakuwa wa kawaida zaidi, na ubinadamu wake unakuwa wa kawaida kabisa. Watu wanapata maarifa mengi ya tabia yao potovu ya kishetani, na iliyopotoka, na asili ya mwanadamu, na pia wanapata shauku kubwa ya kuuelewa ukweli. Hiyo ni kusema, maisha ya mwanadamu yanakua zaidi na zaidi, na tabia upotovu ya mwanadamu inakuwa na uwezo wa mabadiliko zaidi na zaidi—yote hiyo ni maana ya Mungu kuwa maisha ya mwanadamu. Kama njia haiwezi kufunua vitu hivyo ambavyo ni asili ya mwanadamu, haiwezi kubadilisha tabia ya mwanadamu, na, zaidi ya hayo, haiwezi kumleta mbele ya Mungu au kumpa ufahamu wa kweli juu ya Mungu, na hata kufanya ubinadamu wake kuwa duni zaidi na hisia zake kuwa si za kawaida zaidi, basi njia hii itakuwa si njia ya kweli, na inaweza kuwa ni kazi ya roho mchafu, au njia ya zamani. Kwa ufupi, haiwezi kuwa kazi ya sasa ya Roho Mtakatifu. Mmemwamini Mungu kwa miaka yote hii, halafu bado hamna uwezo wa kutofautisha kati ya njia ya kweli na njia ya uongo au kuweza kuitafuta njia ya kweli. Watu wengi hawana haja na masuala haya; wanakwenda tu kule ambako wengi wanakwenda, na wanarudia kile ambacho watu wengi wanasema. Mtu kama huyu anawezaje kuwa mtu anayetafuta njia ya kweli? Na watu kama hao wanaweza kuipata njia ya kweli? Ukielewa kanuni hizi muhimu, basi chochote kitakachotokea hutadanganywa. Leo, ni muhimu sana kwamba mwanadamu awe na uwezo wa kutofautisha mambo; hiki ndicho kinapaswa kuwa katika ubinadamu wa kawaida, na kile ambacho mwanadamu anapaswa kuwa nacho katika uzoefu wake. Ikiwa hata leo, mwanadamu bado hawezi kutofautisha kitu katika ufuataji wake wa ukweli, na hisia zake za kibinadamu bado hazikui, basi mwanadamu ni mpumbavu sana, na njia yake ni makosa na imepotoka. Hakuna tofauti hata ndogo katika maisha yako leo, na ingawa ni ukweli, kama unavyosema, umepata njia ya kweli, ni kweli umeipata? Umeweza kuwa na uwezo wa kutofautisha kitu chochote? Kiini cha njia ya kweli ni nini? Katika njia ya kweli, bado hujapata njia ya kweli, hujapata kitu chochote cha ukweli, yaani, hujapata kile ambacho Mungu anataka kutoka kwako, hivyo hakujawa na tofauti katika upotovu wako. Ukiendelea kufuatilia kwa njia hii, hatimaye utaondolewa. Baada ya kufuata hadi leo, unapaswa kuwa na hakika kwamba njia ambayo umechukua ndiyo njia sahihi, na usiwe na shaka zaidi. Watu wengi siku zote wanakuwa hawana uhakika na wanashindwa kufuatilia ukweli kwa sababu ya masuala fulani madogo madogo. Watu kama hao ni wale ambao hawana ufahamu ya kazi ya Mungu, ni wale ambao wanamfuata Mungu katika mkanganyiko. Watu ambao hawaijui kazi ya Mungu hawawezi kuwa wandani Wake, au kuwa na ushuhuda Kwake. Ninawashauri wale ambao wanatafuta tu baraka na kufuata kile ambacho si dhahiri na dhahania wafuatilie ukweli mapema iwezekanavyo, ili kwamba maisha yao yaweze kuwa na maana. Msiendelee kujidanganya tena!

Iliyotangulia:  Ni Jinsi Gani Ambavyo Mwanadamu Ambaye Amemwekea Mungu Mipaka katika Fikira Zake Anaweza Kupokea Ufunuo wa Mungu?

Inayofuata:  Tofauti Kati ya Huduma ya Mungu Mwenye Mwili na Wajibu wa Mwanadamu

Mipangilio

  • Matini
  • Mada

Rangi imara

Mada

Fonti

Ukubwa wa Fonti

Nafasi ya Mstari

Nafasi ya Mstari

Upana wa ukurasa

Yaliyomo

Tafuta

  • Tafuta Katika Maneno Haya
  • Tafuta Katika Kitabu Hiki

Connect with us on Messenger